News & Events

Serikali yatoa bilioni 5 kukabiliana na uhaba wa maji Mkoa wa Dodoma

Waziri wa Maji Mhe.Jumaa Aweso,akizungumza mara baada ya kukagua Mradi wa Maji wa Buigiri akiwa na Kamati ya Kidumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji chini ya Mwenyekiti wake, Christina Shengoma pamoja na Viongozi wa Wizara ya Maji.Waziri wa Maji Mhe.Jumaa Aweso,akizungumza mara baada ya kukagua Mradi wa Maji wa Buigiri akiwa na Kamati ya Kidumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji chini ya Mwenyekiti wake, Christina Shengoma pamoja na Viongozi wa Wizara ya Maji.
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji wakikagua mradi wa Maji wa Bugiri Chamwino mkoani Dodoma walipoambatana na Viongozi wa Wizara ya Maji chini ya Waziri wa Maji, Jumaa Aweso.

DODOMA:
.........................................................................................

Jumla ya Shilingi bilioni tano zimetolewa na Serikali kwa ajili ya kutatua na kupunguza adha ya huduma ya maji katika Mkoa wa Dodoma ambapo Fedha hizo zimetumika kuboresha miundombinu ya maji, pamoja na uchimba visima vya ziada vya maji.

Hayo yamebainishwa Jijini Dodoma na Waziri wa Maji Mhe. Jumaa Aweso wakati wa ziara ya Kamati ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji ya kukagua hali ya upatikanaji wa maji katika jiji la Dodoma na Wilaya ya Chamwino.

Mhe.Aweso amemshukuru Rais Samia kwa kuwapatia Sh Bilioni Tano kwa ajili ya miradi ya maji mkoani Dodoma huku akieleza hadi sasa tayari washachimba visima 10, vitatu kati ya hivyo vikiwa ni vikubwa na kimoja kitakua na uwezo wa kuchukua Lita Laki Nne kwa saa.

 “Visima 10 tayari vimeshachimbwa ikiwamo vitatu vikubwa na Wizara ya maji imeanza kutathmini mradi wa maji kutoka Ziwa Victoria hadi mkoani Dodoma na pia mradi wa bwawa la Farkwa nao upo kwenye hatua ya kuanza utekelezaji wake, lengo ni kuhakikisha Dodoma inakuwa na maji ya kutosheleza,” amesema Aweso.

” Kwanza niishukuru Kamati yetu ya kudumu ya Bunge kwa kutembelea na kukagua miradi yetu, niwatoe hofu serikali kupitia Wizara yetu ya Maji tunashughulikia kwa karibu changamoto ya maji Mkoa wa Dodoma na tayari tumeshaanza mikakati ya kuvuta Maji kutoka Ziwa Viktoria ambapo tunaamini na Bwawa letu la Farkwa likikamilika basi shida itakua imeisha Dodoma

Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Dkt. Christine Ishengoma, amebainisha kuwa kamati imeridhishwa  na jitihada zilizochukuliwa na Wizara pamoja na Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Dodoma (DUWASA) kuhakikisha wanamaliza kero ya uhaba wa maji.

“Hatua mnazozichukua ni nzuri na zinatia moyo tunaamini kuwa tutapata maji ya kutosha katika Jiji la Dodoma na Mkoa wa Dodoma kwa ujumla,” amesema Dkt.Ishengoma

Awali, Mkurugenzi wa DUWASA, Mhandisi Aron Joseph, amebainisha kuwa miongoni mwa miradi inayotekelezwa ni ujenzi wa tenki la kuhifadhia maji la Buigiri Wilaya ya Chamwino lenye uwezo wa kuhifadhi lita za ujazo milioni 2.5 ambazo zitahudumia Wilaya yote, eneo la Ikulu na mji wa kiserikli.

“Mradi huu ulikuwa na thamani ya Sh.Bilioni 2.5 lakini umetekelezwa kwa Sh.Milioni 998 kwa maelekezo ya Wizara kwamba tuhakikishe tunapunguza gharama za utekelezaji wa miradi na tumefanikiwa kwa kuwa tupo asilimia 98 ya utekelezaji wa mradi huu wa tenki,” amesema.

  • Google+
  • E-mail
  • PrintFriendly